banner

October 15, 2019

KUFUZU EURO 2020, MAMBO YANAZIDI KUPAMBA MOTO, ANGALIA NDANI YA STARTIMES

KUFUZU EURO 2020, MAMBO YANAZIDI KUPAMBA MOTO, ANGALIA NDANI YA STARTIMES




Na Mwandishi Wetu
MECHI ya mwisho, England wametoka uwanjani kwa machungu wakiwa ugenini dhidi ya Jamhuri ya Czech ambao waliwatwanga kwa mabao 2-1 katika mechi ya kuwania kufuzu kucheza michuano ya Euro 2020 ambayo itakuwa na mfumo wake mpya kabisa.

Mechi hizo ambazo kwa sasa ni gumzo katika soka la Ulaya, zinaonyeshwa moja kwa moja katika king’amuzi cha StarTimes ambacho kinatumia mfumo wa HD, yaani High Definition.

StarTimes wamekuwa wakionyesha mechi hizo na kila baada ya kuwa zimechezwa kunakuwa na marudio kadhaa kuwapa nafasi wapenda soka ambao walikuwa wanaangalia mechi fulani kwenda kuangalia mechi nyingine ambazo hawakuona.

Burudani imekuwa tamu, England wao watarejea kujiuliza tena uwanjani kutokana na kilichowatokea, kipigo dhidi ya Jamhuri ya Czech ambao walifanya sherehe kubwa.

England wao wanarejea uwanjani leo, safari hii wakiwa ugenini tena dhidi ya Bulgaria, hii ni safari nyingine ngumu kwao kabla hawajarejea nyumbani Alhamisi dhidi ya Montenegro na matumaini makubwa yakiwa ni kushinda, hakuna mjadala.

Kabla ya wao hawajarudi uwanjani, wapenda mpira leo watakuwa wanaburudika na StarTimes kushuhudia mechi kadhaa za Kundi A, B na H.

Moja ya mechi ya England dhidi ya Bulgaria itatupiwa macho sana kwa kuwa wao kupoteza mechi mbili mfululizo, itakuwa ni ‘dhambi’ kubwa wadau wa soka la England na wanachotaka si sare zaidi ya ushindi.

England wanaamini timu yao ina uwezo mkubwa sana, wanataka kushinda na si jambo jingine. Lakini Bulgaria nao wasingependa kuonekana ni mchekea au ngazi huku wenzao waliweza kuwaangusha England, hivyo wangependa kufanya hivyo wakiwa nyumbani kwao pia.

Mfumo ya kuwania kufuzu kucheza Euro 2020, kidogo imekuwa na ugumu tofauti na awali. Mechi ni nyingi na zinachezwa karibukaribu, hivyo kila timu inalazimika kujiandaa sana.

Kunakuwa na mzigo mzito kwa timu kama ya England ambayo kama imepoteza mchezo mmoja ugenini, inakwenda tena kucheza ugenini, presha inakuwa maradufu.

Hii ni kwa kuwa watalazimika kuchukua presha mara mbili kwa kuwa kucheza ugenini kawaida presha inaongezeka na hasa kama timu inayopaniwa na wengi kutokana na ukubwa wa taifa hilo na historia ya soka.

Pamoja na hivyo, Kocha Mkuu wa England, Garry Southgate anaamini mambo yatakuwa mazuri na lakini anaijua pia hofu ya kupoteza mchezo mwingine wa pili, England ni presha kubwa.

Pamoja na hivyo, kikosi cha Ureno chini ya Nahodha Cristiano Ronaldo nacho kitarudi uwanjani. Hii ni baada ya mechi iliyopita ambayo walishinda kwa mabao 3-0 dhidi ya Luxembourg.

Ronaldo ameishaeleza namna anavyokiamini kikosi chake, anaona wanavyoweza kufanya kweli licha ya ugumu wa michuano hiyo.

Mfumo wa michuano hiyo kuwa mpya, kuchezwa katika nchi 12 na miji 12 tofauti kwa mwezi mzima, inaonekana ni burudani inayosubiriwa kwa hamu kubwa.

Kila upande unataka kuingia kwenye rekodi hiyo ya kucheza michuano hiyo katika miji tofauti na nchi tofauti. Hii nayo imekuwa ikiongeza presha kwa kiasi kikubwa.

Unaona, tayari kuna makocha wako katika presha kubwa akiwemo Southgate kwa kuwa kuna mataifa kawaida huonekana hayastahili kukosa michuano hiyo au mingine yoyote kama vile Kombe la Dunia.

Sweden dhidi ya Hispania kesho, ni mechi nyingine inayosubiriwa kwa hamu kubwa kama ilivyo kwa Ufaransa na Uturuki.

Licha ya kutokuwa na rekodi kubwa Ulaya, Uturuki wanajulikana kama “Taifa sumbufu” hasa wanapokutana na vigogo.

Michuano hii, wachezaji wanaotokea katika ligi mbalimbali maarufu wanakuwa wameingia katika presha tofauti. Wako wanaotegemewa lakini wanakutana na vikosi vyao ambavyo ni dhaifu tofauti na klabu zao na wanalazimika kufanya kazi ya ziada.

Bado wako wenye bahati, wanakutana na vikosi vyao vikiwa bora na wanapata nafasi ya kung’ara zaidi. Kumbuka, hatua hii ya kufuzu Euro 2020 inakuwa na “surprise” za kutosha.


LEO
KUNDI A
Bulgaria Vs England
Kosovo Vs Montenegro


KUNDI B
Ukraine Vs Ureno
Lithuania Vs Serbia


KUNDI H
Ufaransa Vs Uturuki
Iceland Vs Andorra
Moldova Vs Albania
KESHO:

 KUNDI D
Swiss Vs Jamhuri ya Ireland
Sweden Vs Hispania
Romania Vs Norway
Faroe Vs Malta

KUNDI G
Israel Vs Latvia

KUNDI J
Liechtenstein Vs Italia
Ugiriki Vs Bosnia & Herzogovina
Finland Vs Armenia







Post a Comment

Whatsapp Button works on Mobile Device only

Start typing and press Enter to search